Tanzania logo

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

SILLO AWATAKA VIONGOZI WA DINI KULINDA AMANI NA MAADILI



SILLO AWATAKA VIONGOZI WA DINI KULINDA AMANI NA MAADILI 


Na Mwandishi Wetu;-


Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Daniel Sillo amewataka viongozi wa dini nchini Tanzania kuendelea kukemea vitendo vya ukiukwaji wa maadili katika jamii na visivyoendana na neno la Mungu ili kulinda mila na desturi nzuri za nchi yetu na kujenga taifa lenye upendo na amani


Sillo amesema hayo katika Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 150 ya Utume Ulimwenguni yaliyofanyika katika kanisa la Waadventista wa Sabato (SDA ) lililopo Mamba Myamba wilayani Same, mkoani Kilimanjaro leo Agosti 29, 2024


Amesema kuwa viongozi wa  dini wanatakiwa kujihusisha katika kuendelea kulinda amani ya nchi yetu na kufanya amani ya nchi kuwa jambo la kwanza 


"Ikiwa tunawafundisha watu kumtii Mungu ambaye ni chanzo cha amani ya kweli basi tunapaswa kuwafundisha waumini umuhimu wa kuendelea kuilinda amani". Amesema 


Aidha Mhe. Sillo alitumia nafasi hiyo kuwahamasisha Wananchi kuwa Mwaka huu mwezi Novemba kutakuwa na uchaguzi wa Serikali za Mitaa hivyo wajitokeze kwa wingi kujiandikisha na kuhuisha taarifa zao katika daftari la Wapiga kura


Kwa upande wake Askofu wa Kanisa la Waadvestista Wasabato Jimbo kuu la Kaskazini mwa Tanzania,  Mark Malekana  ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa ushirikiano mzuri wanaoutoa kwa viongozi wa dini, aliongeza kuwa kanisa litaendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali katika masuala ya Ustawi wa Jamii ili amani iendelee kutamalaki na kujenga taifa lenye ustawi